Monday, August 22, 2011

VODACOM MISS TANZANIA NDANI YA V-HOUSE

Warembo wanaoshiriki shindano la Vodacom Miss Tanzania 2011 wakiwa katika picha ya pamoja. Warembo hawa wamerejea jana katika jumba la Vodacom baada ya kumaliza ziara yao ya siku kumi kutembelea mbuga za wanyama za Mikumi, mji wa Monduli, Ngongoro, Tarangire, Arusha mjini kuhamasisha utalii wa ndani nchini pamoja na kufanya shughuli mbalimbali za kijamii wakiwa katika ziara hiyo.
Vodacom Miss Tanzania wamaliza ziara yao kanda ya Kaskazini.

Washiriki 30 wa shindano la Vodacom Miss Tanzania waliokuwa kwenye ziara ndefu ya kimafunzo mikoa ya Morogoro, Kilimanjaro na Arusha wamemaliza ziara hiyo na wamerejea ndani ya jumba lao 'Vodacom House'.

Ziara hiyo ya mafunzo iliyochukua takribani siku kumi iliwafikisha walimbwende hao kwenye Hifadhi za Taifa za Mikumi, Ngorongoro, Tarangire na shule ya wasichana ya Maasai iliyopo wilayani Mbonduli.

Meneja Uhusiano na Habari za Mtandao wa Vodacom Tanzania Matina Nkurlu aliyataja maeneo mengine waliyotembelea kuwa ni shule ya watoto wa kimaasai Monduli, Kaburi la hayati Moringe Sokoine, kiwanda cha Bia TBL tawi la Arusha na mitambo ya simu ya Kampuni ya Vodacom ambao ndio wadhamini wakuu wa shindano hilo.

Akiielezea ziara hiyo ya mafunzo aliyoiita ya mafanikio, Nkurlu amesema warembo hao wamepata fursa ya kujifunza mengi hususani kuhusiana na utalii wa ndani.

“Tumemaliza salama ziara hii ya mafunzo iliyowapa zaidi ufahamu walimbwende hawa kuhusiana na historia na rasilimali zilizopo nchini. Washiriki wamejionea maeneo mbalimbali ya kitalii ikiwemo Ngorongoro Crater ambapo wanyama pori na binadamu wanaishi katika eneo moja,” alisema.

Nae Mkurugenzi wa kampuni ya Lino Agency ambao ndio waandaaji wa shindano hilo Hashim Lundenga alisema, baada ya kuwasili washiriki hao 30 walipata fursa ya kukutana na ndugu, jamaa na marafiki katika siku ya familia iliyoandaliwa na Vodacom Tanzania ambao ndio wadhamini wakuu wa shindano hilo.

“Baada ya ziara ndefu Morogoro na kanda ya kaskazini, warembo wamekutana na jamaa zao kwa mazungumzo kabla hatujaingia kwenye hatua ya mwisho ya kumtafuta mshindi. Ni matarajio yetu wataitumia elimu waliyoipata katika kuvitangaza vema vitutio vya utalii vilivyopo nchini huko waendako,” alisema Lundenga.

Kwa upande wake mrembo Jennifer Kakolaki alisema anajivunia kuwa mmoja wa washiriki wa Vodacom Miss Tanzania 2011 kwani hata baada ya kumalizika kwa shindano hilo anaweza kutumia elimu waliyoipata kujitafutia ajira kupitia sekta hiyo ya utalii.

“Kiukweli tumejifunza mengi kwenye ziara yetu, nawashukuru waandaaji na Kampuni ya Vodacom kwa kuona umuhimu wa kutuandalia ziara hii ikiwemo kutupatia muda wa kukutana na familia zetu. Kwa niaba ya wenzangu naahidi hatutawaangusha na tutafanya tulichojifunza,” alisema Kakolaki

Mwaka huu warembo hao wameingia kambini kwa mfumo tofauti na uliozoeleka kwani wanaishi kwenye jumba maalum la Vodacom ambapo matukio yao yatakuwa yakioneshwa kupitia Startv na Clouds TV na watazamaji watapata fursa ya kupiga kura kuchagua mrembo
watakayemuona anafaa.

Na Global Publishers Tz

No comments:

Post a Comment