Monday, July 30, 2012

Saintfiet amuita Sure Boy Yanga


KOCHA Mkuu wa Yanga, Tom Saintfiet, amekubali kiwango cha kiungo wa Azam FC, Salum Abulbakar ‘Sure Boy’ na yupo tayari kumuongeza kwenye kikosi chake.

Kauli hiyo ameitoa baada ya kumalizika kwa fainali ya Kombe la Kagame juzi kwenye Uwanja wa Taifa na Yanga kushinda mabao 2-0, ingawa kiungo huyo alionyesha kiwango cha kuvutia.

Akizungumza na Championi Jumatatu, Saintfiet alisema amemfuatilia Sure Boy kwa muda mrefu tangu michuano hiyo ilipoanza na kuridhika kwamba kiwango chake ni kizuri.

Saintfiet alisema kiungo huyo ana uwezo wa kupiga pasi na kumiliki mpira na ndiye kiungo aliyemvutia katika michuano hiyo kutokana na aina yake ya uchezaji.

Alisema yupo tayari kutoa mapendekezo kwa uongozi wa klabu hiyo kongwe kumsajili kutokana na kucheza soka linaloendana na mfumo anaoufundisha.
“Kama kuna mchezaji ambaye alinivutia basi ni Salum (Abulbakar-Sure Boy), ana kiwango kikubwa na yupo makini katika upigaji wake wa pasi na kumiliki mpira.

“Nipo tayari kukutana na viongozi kuwashawishi kumsajili kiungo huyo, ndiye aliyetusumbua na kutupa wakati mgumu katika fainali yetu dhidi ya Azam,” alisema Saintfiet.

Na Wilbert Molandi, GPL

No comments:

Post a Comment